UKURASA WA 765; Weka Macho Yako Fedha Zako Zilipo…

By | February 3, 2017

Chunga sana fedha zako, hili ni hitaji muhimu kama unataka kufanikiwa kifedha.

Hakikisha macho yako yapo pale fedha zako zilipo, kwa sababu kama wewe hutakuwa makini na fedha zako, basi jua hakuna anayeweza kuwa makini na fedha hizo.

Wapo watu wengi ambao wanaweka fedha zao kwenye biashara, lakini wanashindwa kusimamia biashara hizo vizuri, mwishowe wanaishia kupata hasara.

Unaposhindwa kusimamia biashara yako vizuri, unapowaacha wengine wafanye maamuzi wanayotaka na biashara yako, unaonesha udhaifu mkubwa. Watu hao wanajifunza kwamba wewe hujali sana kuhusu biashara yako na hivyo wanaweza kufanya chochote wanachotaka.

SOMA; Zipo Fedha Za Kutosha Kila Mtu Kuwa Bilionea…

Popote ulipoweka fedha zako, hasa kwenye biashara, fuatilia kwa karibu sana. Hakikisha wewe ndiye mwamuzi wa mwisho kwenye kila kinachofanyika. Hata kama una wasaidizi unaowaamini kwa kiasi gani, hata kama una ndugu wa karibu anayesimamia biashara hizo, hakikisha wewe unabaki kuwa mwamuzi mkuu wa mambo muhimu ya biashara hiyo.

Usikwepe jukumu hili kwa kisingizio chochote kile, hata kama muda unakubana, hakikisha macho yako yapo kwenye fedha zako.

Ninakuambia hivi kwa sababu watu wengi wamepoteza fedha zao kwa uzembe wao wenyewe. Wanajisahau na kuwaacha wengine wawe na maamuzi makubwa kwenye fedha zao, hasa kwa upande wa biashara. Na watu wanapoanza kuzoea hali hiyo, wanajikuta wanafanya maamuzi ambayo yanakutana na changamoto. Hapo ndipo mnapoanza kuja kulaumiana na kuona wengine wamekuletea hasara.

Lakini chanzo halisi ni wewe kushindwa kuchunga fedha zako, chanzo ni wewe kutoa macho yako kwenye fedha zako. Usifanye kosa hili, utakuja kuwalaumu wengine bure kwa uzembe uliotengeneza wewe.

Hakikisha macho yako kwenye fedha zako, muda wowote ule.

Kila la Kheri Rafiki Yangu.

Rafiki na Kocha wako,

Makirita Amani,

Kwa ushauri na Coaching bonyeza maandishi haya kupata utaratibu.

Kwa kupata vitabu vya biashara na mafanikio tembelea MOBILE UNIVERSITY (bonyeza hayo maandishi.)

Kupata blog ya kitaalamu unayoweza kuitumia kutengeneza kipato tembelea MTAALAMU NETWORK

Category: KURASA ZA MAISHA

About Dr. Makirita Amani

Dr. Makirita Amani ni daktari wa binadamu, mwandishi, mhamasishaji na mjasiriamali. Dhumuni lake kubwa kwenye maisha ni KUWASAIDA WATU KUBORESHA MAISHA YAO NA KUFIKIA MAFANIKIO MAKUBWA KUPITIA KAZI ANAZOFANYA. Mawasiliano 0717396253 email makirita@kisimachamaarifa.co.tz

One thought on “UKURASA WA 765; Weka Macho Yako Fedha Zako Zilipo…

  1. Pingback: UKURASA WA 769; Jinsi Ya Kuongeza Bahati Yako Ya Kufanikiwa… – Kisima Cha Maarifa

Leave a Reply

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.