UKURASA WA 894; Kushindana Na Watu Bilioni Saba…

By | June 12, 2017

Unahitaji kuwa bora zaidi kwenye kile ambacho unakifanya, bora kabisa duniani, kwa kuweza kukifanya kwa namna ambavyo hakijawahi kufanywa na yeyote duniani. Lakini changamoto ni kwamba, dunia ina watu zaidi ya bilioni saba, na karibu wote wanakazana kufanya vitu vile vile ambavyo vinafanana. Hili linapelekea ushindani kuwa mkali, watu bilioni saba siyo mchezo.

Kwa wingi huu wa watu, wengi wanapotezwa na hawasikiki wala kuonekana wanafanya nini, licha ya maendeleo makubwa ya kiteknolojia yanayoweza kumfanya kila anayefanya kitu bora aonekane.

Huenda unafikiri hapa kwamba inabidi uwe na fedha nyingi, uwezo mkubwa na akili nyingi kuweza kuwa bora zaidi ya watu wote bilioni saba. Lakini hapo unajidanganya, unafanya kitu rahisi kionekane kigumu.

Iwapo kila mara utafikiria na kutafuta njia mpya za kuwasaidia watu, hutakuwa tena na haja ya kushindana na watu bilioni saba. Kwa kufikiria njia hizo mpya mara zote unakuwa mbele ya wengine, kwa sababu wengi wanafanya yale waliyozoea. Kuwa na njia mpya kunakuweka mbele, kuna na njia mpya zinazowasaidia wengine, kunaifanya dunia ikujue.

SOMA; Kuhusu Kupambana, Kushindana Na Kubishana…

Kwa njia hii unaweza kuonekana wa ajabu, unaweza kuonekana unafanya mambo ya ajabu, lakini baadaye utakuja na njia bora zaidi, zitakazowasaidia wengi zaidi. Ni lazima uwe na ujasiri wa kuweza kufanya hayo ya tofauti, ambayo wengine bado hawajayaona.

Usishindane na watu bilioni saba, ni jambo la kijinga kufanya na halitakusaidia chochote. Badala yake angalia njia mpya za kuwasaidia watu, kufanya maisha yao kuwa bora zaidi na utakuwa mbele ya watu bilioni saba.

Kila la Kheri Rafiki Yangu.

Rafiki na Kocha wako,

Makirita Amani,

Kwa kupata vitabu vya biashara na mafanikio tembelea www.kisimachamaarifa.co.tz/vitabu

Kupata blog ya kitaalamu unayoweza kuitumia kutengeneza kipato tembelea www.mtaalamu.net/patablog

Category: KURASA ZA MAISHA

About Dr. Makirita Amani

Dr. Makirita Amani ni daktari wa binadamu, mwandishi, mhamasishaji na mjasiriamali. Dhumuni lake kubwa kwenye maisha ni KUWASAIDA WATU KUBORESHA MAISHA YAO NA KUFIKIA MAFANIKIO MAKUBWA KUPITIA KAZI ANAZOFANYA. Mawasiliano 0717396253 email makirita@kisimachamaarifa.co.tz

Leave a Reply

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.