UKURASA WA 940; Kuna Kitu Unaweza Kufanya…

By | July 28, 2017

Tofauti ya wale wanaoweza kufanya makubwa licha ya kuwa na changamoto na wale wanaokata tamaa na kuacha, siyo ukubwa wa changamoto, wala siyo uwezo wa kifedha au kiakili, bali ni tofauti ya mtazamo.

Wale wanaokata tamaa na kuacha ni wale ambao wakikutana na changamoto wanajiambia hakuna ninachoweza kufanya. Nimejaribu sana lakini imeshindikana. Hakuna tena namna, inabidi nifanye kitu kingine. Safari inaishia hapo na hakuna kikubwa wanaweza kufanya.

Lakini wale wanaofanya makubwa, wale wanaovuka changamoto na kupata matokeo makubwa, wanapokutana na ugumu wanajiambia kuna njia ya kupita hapa, kuna kitu wanaweza kufanya. Na licha ya kujaribu na kushindwa, ule mtazamo wa kwamba kuna kinachoweza kufanyika huwa hautoki ndani yao. Na kweli inafika hatua wanaona kitu cha kufanya, au wanajaribu njia fulani na ndiyo inayoleta majibu.

SOMA;  Usikimbilie Kufanya Vitu Rahisi, Vitakupoteza Kibiashara…

Sasa turudi kwako rafiki, unapokutana na hali yoyote ngumu au ya changamoto, kipi unachoanza kufikiria haraka? Unafikiria kwamba ndiyo mwisho na haiwezekani tena? Au unafikiria ipo njia ya kuweza kufanya, kipo kitu cha kufanya?

Anza sasa kufikiria kwamba ipo njia, hata pale wengine wote wanaposema hakuna njia, wewe sema ipo njia. Hata kama huna uhakika kwamba njia inatoka wapi, wewe amini ipo njia, na endelea kuweka juhudi kuhakikisha unaifikia njia hiyo.

Kwa mtazamo huu, mara zote utapata njia ya kutatua lolote unalokutana nalo. Na hata kama hutalitatua kabisa, angalau utapata njia mbadala ya kufika au kupata kile unachotaka.

Kila la Kheri Rafiki Yangu.

Rafiki na Kocha wako,

Makirita Amani,

Kwa kupata vitabu vya biashara na mafanikio tembelea www.kisimachamaarifa.co.tz/vitabu

Kupata blog ya kitaalamu unayoweza kuitumia kutengeneza kipato tembelea www.mtaalamu.net/patablog

Category: KURASA ZA MAISHA

About Dr. Makirita Amani

Dr. Makirita Amani ni daktari wa binadamu, mwandishi, mhamasishaji na mjasiriamali. Dhumuni lake kubwa kwenye maisha ni KUWASAIDA WATU KUBORESHA MAISHA YAO NA KUFIKIA MAFANIKIO MAKUBWA KUPITIA KAZI ANAZOFANYA. Mawasiliano 0717396253 email makirita@kisimachamaarifa.co.tz

Leave a Reply

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.