UKURASA WA 851; Ni Matatizo Gani Unayotatua?

By | April 30, 2017

Swali muhimu mno kujiuliza kila wakati na kwa kila jambo unalofanya. Usifanye tu kwa sababu wengine wanafanya, wala usifanye ili uonekane na wewe unafanya. Swali la msingi ni tatizo au matatizo gani unayotatua? Ukianzia hapo, utaziona fursa nyingi sana, ambazo tayari zinakuzunguka ila tu wewe huzioni.

IMG-20170321-WA0000

Kama unamiliki biashara, je ni matatizo gani biashara yako inatatua? Biashara yako inafanyaje maisha ya wengine kuwa bora zaidi ya yalivyo sasa? Thamani gani kubwa zaidi unaongeza kwa wengine? Hapo ndipo pa kuanzia na kadiri unavyofikiria na kujiuliza hivyo, ndivyo unavyoona fursa zaidi za kuwasaidia watu na wewe kunufaika zaidi.

Kama umeajiriwa, ile kazi ambayo wewe unaifanya, ni matatizo gani unayotatua? Ni thamani gani unaongeza kwa wengine? Anayetegemea unachofanya ananufaikaje? Aliyekuajiri naye ananufaikaje? Lazima uanze na maswali haya, kabla hata hujaanza kulalamika kwamba kipato ni kidogo. Maana ukiyajua maswali haya vizuri, na ukaweza kuyafanyia kazi, utatatua matatizo mengi zaidi na kuweza kuongeza thamani zaidi, itakayopelekea ulipwe zaidi.

SOMA; Dawa Moja Inayotibu Matatizo Yako Yote….

Moja ya matatizo ninayotatua mimi, ni kuwasaidia watu waweze kutatua matatizo mengi zaidi kwenye maisha yao, kazi zao na biashara zao. Kwa sababu kila eneo la maisha lina changamoto zake, watu wanapoweza kuzivuka changamoto hizo, basi wanaweza kutoa thamani kubwa kwa wengine. Watu wanapokuwa na nidhamu nzuri ya fedha, wanapowekeza, wanapotumia muda wao vizuri, wanapojifunza kila siku, wanapofanya kitu kinachoongeza thamani kwa wengine, wanaondokana na matatizo mengi na wengi wananufaika.

Kwa watu kuweza kuondokana na matatizo yao, wanatengeneza mafanikio zaidi kwao na kwa wengine pia.

Swali muhimu la kujiuliza na kujipa majibu ni je unatatua matatizo gani?

Nijibu kwenye sehemu ya maoni hapo chini ili tuweze kujadiliana kwa kina.

Karibu sana.

Kila la Kheri Rafiki Yangu.

Rafiki na Kocha wako,

Makirita Amani,

Kwa ushauri na Coaching bonyeza maandishi haya kupata utaratibu.

Kwa kupata vitabu vya biashara na mafanikio tembelea MOBILE UNIVERSITY (bonyeza hayo maandishi.)

Kupata blog ya kitaalamu unayoweza kuitumia kutengeneza kipato tembelea MTAALAMU NETWORK

Category: KURASA ZA MAISHA

About Dr. Makirita Amani

Dr. Makirita Amani ni daktari wa binadamu, mwandishi, mhamasishaji na mjasiriamali. Dhumuni lake kubwa kwenye maisha ni KUWASAIDA WATU KUBORESHA MAISHA YAO NA KUFIKIA MAFANIKIO MAKUBWA KUPITIA KAZI ANAZOFANYA. Mawasiliano 0717396253 email makirita@kisimachamaarifa.co.tz

Leave a Reply

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.