UKURASA WA 885; Kipi Watu Hawataki Kufanya?

By | June 3, 2017

Hicho ndiyo unapaswa kufanya wewe.

Ndiyo, kile ambacho watu wengi hawapo tayari kufanya, ndiyo unachopaswa kufanya wewe. Kwa sababu hicho ndiyo kitu unachoweza kujitofautisha nacho na hata kuweza kutengeneza thamani kubwa sana.

Watu wengi hawapo tayari kufanya kazi zao kwa hatua ya ziada, hawapo tayari kuweka juhudi zaidi ili kupata matokeo bora zaidi. Hawapo tayari kuanza kazi mapema zaidi na kuchelewa kumaliza kazi. Wewe fanya hayo, na muda siyo mrefu utajikuta upo mbali kwenye kazi yako ukilinganisha na wengine.

Kwenye biashara, wengi hawapo tayari kuwajali wateja kwanza, wanaangalia faida zaidi. Hawapo tayari kuwapa wateja huduma bora kabisa na za kipekee. Hawapo tayari kuweka juhudi kubwa kujenga biashara itakayodumu muda mrefu. Wewe fanya hayo muhimu, iangalie biashara yako miaka 100 ijayo na siyo mwezi ujao.

Watu wengi hawapo tayari kuweka akiba, hawapo tayari kuanza kuwekeza mapema kwenye maisha yao. Husubiri wakiamini muda bado, na muda unapokuja kufika, wanajikuta wamechelewa na hawana pa kusimamia. Wewe, anza mapema kuweka akiba na kuwekeza. Usijidanganye kwa namna yoyote ile.

SOMA; Kabla Fedha Haijaanza Kukufanyia Kazi….

Yale ambayo wengi hawapendi kufanya, ni mambo magumu, mambo yasiyofurahisha kufanya, lakini pia ndiyo mambo yenye thamani kubwa ukiyafanya. Yafanye mambo haya wewe, na utajitenga na kundi kubwa la watu ambao wanakimbilia kufanya mambo rahisi na yaliyozoeleka. Kwa njia hiyo unajitenga na ushindani na kuandaa misingi imara ya baadaye.

Kila la Kheri Rafiki Yangu.

Rafiki na Kocha wako,

Makirita Amani,

Kwa kupata vitabu vya biashara na mafanikio tembelea www.kisimachamaarifa.co.tz/vitabu

Kupata blog ya kitaalamu unayoweza kuitumia kutengeneza kipato tembelea www.mtaalamu.net/patablog

Category: KURASA ZA MAISHA

About Dr. Makirita Amani

Dr. Makirita Amani ni daktari wa binadamu, mwandishi, mhamasishaji na mjasiriamali. Dhumuni lake kubwa kwenye maisha ni KUWASAIDA WATU KUBORESHA MAISHA YAO NA KUFIKIA MAFANIKIO MAKUBWA KUPITIA KAZI ANAZOFANYA. Mawasiliano 0717396253 email makirita@kisimachamaarifa.co.tz

Leave a Reply

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.